DIEGO Maradona amewataka mashabiki wa Napoli kuelekeza hasira zao kwa bodi ya klabu hiyo baada ya kumruhusu straika wao hatari Gonzalo Higuain kutua kwa mahasimu wao wakubwa, Juventus.
Nyota huyo raia wa Argentina, amekamilisha usajili wa pauni milioni 79 katika kikosi cha Juventus kufuatia kupimwa afya kwa siri jijini Madrid, hatua ambayo imewafanya mashabiki wamkasirikie.

Tayari mashabiki wa klabu hiyo, wameanza kumchana Higuain kwa kutuma picha zenye jezi namba 9 ya straika huyo kwenye Twitter zikimuonyesha akiwa kwenye moto au chooni.
Hata hivyo, Maradona ambaye ni mchezaji wa zamani wa Napoli, amesema mashabiki wanatakiwa kuwakasirikia marais wa timu ambao akili zao zipo kibiashara zaidi.

Katika Mtandao wa Facebook, Maradona aliandika: “Hili suala la Higuain linaniumiza kwa sababu anakwenda kwa wapinzani wa moja kwa moja, Juventus. Lakini hatuwezi kumlaumu mchezaji.  
“Mchezaji anajipigania mwenyewe na ni wale ambao wana tamaa ya biashara ndiyo ambao wamefanikisha kwa kiasi kikubwa suala hili. Hakuna mtu anayefikiria kuhusu mashabiki.”

Post a Comment

 
Top