MATOKEO mabaya ya Yanga katika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho barani Afrika, yanalifikirisha benchi la ufundi la timu hiyo hasa katika mpangilio wa kikosi kwa msimu ujao wa ligi na michuano ya kimataifa.

Yanga juzi ilikubali kipigo cha mabao 3-1 kutoka kwa Madeama ya Ghana, ikiwa ni mchezo wa nne wa Kundi A la michuano hiyo, huku ikiwa timu pekee kwenye kundi lake iliyopoteza mechi tatu na kuambulia sare moja tu.

Mchezo wa juzi ulidhihirisha wazi kwamba Yanga inahitaji kukitazama upya kikosi chake kuanzia aina ya wachezaji wa kigeni ilionao hadi wale wa ndani hasa katika nafasi ya ulinzi na kiungo mkabaji ambazo zinaonekana kupwaya mno.

Haja ya kukiangalia upya kikosi kizima cha Yanga kwa ajili ya faida ya timu hiyo kwenye michuano ya kimataifa, imeonekana baada ya mchezo dhidi ya Madeama ambapo kocha mkuu wa timu hiyo Mholanzi, Hans Van der Pluijm, ameeleza masuala kadhaa ya msingi kwenye timu hiyo.

“Inawezekana nina kikosi kizuri sana, lakini kinafanya makosa ya kila mara ambayo yanaigharimu timu, sasa lazima kuangalia upya kikosi chote, ni kweli hatuna kiungo mkabaji wa uhakika na hili si tatizo la Yanga pekee lakini nadhani Tanzania nzima ukiangalia hakuna kiungo wa kariba hiyo,” alisema kocha huyo.

Pluijm alisema kikosi chake kimeonekana kuwa na upungufu kadhaa na kuahidi atafanya marekebisho makubwa kuelekea michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani.

Pluijm alisema kadiri wanavyocheza mechi hizo za kimataifa anabaini kwamba kuna jambo linahitajika kwenye timu yake ndiyo maana anasisitiza usajili wa uhakika utakaoihakikishia Yanga nafasi ya kuwa timu bora zaidi msimu ujao.

“Labda tuangalie namna tunavyosajili sasa, ni kweli tuna kikosi kizuri lakini tujiulize upya ni kizuri kwa maana ipi? Kwa ligi ya ndani au michuano ya kimataifa? Naamini timu yangu iko vizuri lakini inapungukiwa vitu muhimu ambavyo sasa lazima tuvivalie njuga,” alisema.


Alisema safu ya ushambuliaji inapoteza nafasi nyungi sana, anahitaji mtu mwenye kulijua lango vizuri licha ya kwamba kuna Donald Ngoma, Obrey Chirwa, Amissi Tambwe, Malimi Busungu na Matheo Anthony.

Pluijm alisema kuelekea katika michuano mwakani, Yanga inahitaji aina ya mshambuliaji mwenye uwezo wa kupambana na mabeki na pia kuwa na mshambuliaji mwenye shabaha ya kufunga mabao na ambaye anaweza kubadilisha matokeo wakati wowote.

Alisema Yanga ina kikosi kipana chenye wachezaji nyota, lakini kuelekea katika michuano ya kimataifa kinahitaji kuwa na watu wa kazi wa kuleta matokeo mazuri.

“Kiungo mkabaji hili halina ubishi, lazima nipate mtu wa kazi, mrefu na mwenye nguvu na nidhamu ya kucheza nafasi hiyo, upande wa kulia pia kunahitajika kuongezwa nguvu. Na eneo la ulinzi la kati nalo linahitaji maboresho kwa sasa hasa kuelekea michezo ya kimataifa mwakani,” alisema.

Alisema ni lazima kikosi chake kifanye usajili wa nguvu katika eneo la beki wa kushoto, mabeki wa kati na kiungo mkabaji nafasi ambazo zimekuwa zikipwaya mara kadhaa hasa wanapokutana na timu ngumu kwenye mechi za kimataifa.

Post a Comment

 
Top