MOJA ya tatizo lililochangia jicho moja la Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano cha Simba, Haji Manara kushindwa kuona ni damu kuganda.
Taarifa kutoka nchini jijini New Delhi, India zimesema, katika vipimo vya awali imegundulika damu iliganda ndani ya jicho hilo na kusababisha kushindwa kwenda katika mzunguko wa kawaida.
 “Wamesema tayari wamempa dawa za mwanzo baada ya vipimo hivyo lakini baada ya hapo kesho (leo), atachukuliwa vipimo zaidi,” alisema Mtanzania anayeishi jijini Delhi ambaye amekuwa karibu na Manara.

 “Tulikwenda kumuona, wametupa taarifa hizo lakini wamesema matibabu yameanza na wana matumaini makubwa ataweza kuona tena. Lakini vipimo vingine vitachukuliwa kwa uhakika zaidi.”
Manara mwenyewe alipatikana baadaye na kusema kweli ameanza matibabu.
“Ninashukuru kwa kuwa nimeanza matibabu na nimeelezwa mambo mengi sana, hivyo acha nimalize vipimo vya kesho (leo) halafu ninaweza kuelezea zaidi.
“Lakini wamesema kuna matumaini ingawa ni tiba inayohitaji uvumilivu kwa kuwa ina mambo mengi sana,” alisema Manara, jana jioni.
Manara hivi karibuni aliamka jicho lake likiwa limepoteza uwezo wa kuona na tiba yake inatarajia kutumika zaidi ya Sh milioni 22.


Post a Comment

 
Top