WAKATI ishu ya Mohammed Dewji kutaka kununua hisa za Simba 51% kwa bilioni 20 ikiwa bado inazunguka kwenye vichwa vya Wekundu hao, kuna ishu nyingine imeibuka ya kudaiwa kuwa timu hiyo imepewa ofa nono ya udhamini wa Azam TV, inayomilikiwa na mfanyabiashara maarufu nchini, Said Salim Bakhresa.
Imeelezwa kuwa suala hilo kwa sasa limekuwa gumzo ndani ya timu hiyo kukiwa na mijadala mbalimbali kuwa uamuzi upi ni sahihi na kipi bora kwa ajili ya msimu ujao na mafanikio ya Simba kwa miaka ijayo.
Pamoja na hayo, ukiachana na Mo Dewji na Azam TV, pia Kampuni ya TBL kupitia bidhaa yake ya Bia ya Kilimanjaro iliyomaliza mkataba wake wa udhamini na klabu hiyo hivi karibuni nayo imetajwa kuonyesha nia ya kuendelea kufanya kazi na timu hiyo yenye maskani yake Mtaa wa Msimbazi, Kariakoo jijini Dar.
Mtu wa ndani kutoka kwenye sekretarieti ya timu hiyo alilitonya Championi Jumatatu kuhusiana na ishu hiyo akibainisha kuwa kwa sasa kumekuwa na mgawanyiko wa makundi baina ya viongozi hao kila mmoja akiweka hoja mezani kwamba kwa nini waingie mkataba na udhamini fulani na kuachana na mwingine.
Hata hivyo, imeelezwa zaidi kuwa mpaka sasa Azam TV inaonekana kuwa na ushawishi mkubwa wa kuingia mkataba na Simba kutokana na kiasi kikubwa cha fedha kilichotajwa kwa ajili ya udhamini wa klabu hiyo.
“TBL bado wanataka kuendelea na udhamini lakini kuna kikwazo baada ya kujitokeza kwa wadhamini wengine, ukiachana na ishu ya MO pia kuna Azam TV wameleta ofa, kwa hiyo bado kuna migongano hapa katikati, kila mmoja anaweka hoja na bado haijafahamika itakuwaje,” alisema mtoa taarifa huyo.
        Bakhresa wa pili kutoka kushoto
 Baada ya taarifa hizo, gazeti hili lilimtafuta Rais wa Simba, Evans Aveva kulitolea ufafanuzi suala hilo lakini simu yake ya mkononi iliita bila ya kupokelewa.
Alipotafutwa makamu wa rais wa timu hiyo, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ alianza kwa kusema: “Nani amesema tumekataa udhamini wa TBL? Niseme tu kwamba hizo taarifa nyingine sizitambui ila ieleweke kuwa mkataba wetu na TBL unaeleza wazi kwamba hatuwezi kuzungumza na kampuni nyingine mpaka tukubaliane kwamba tumeshindwa kuendelea nao, ieleweke hivyo kwa sasa.”


Post a Comment

 
Top