WAKATI  beki wa kulia wa Yanga, Hassan Kessy akiendelea kufanya mazoezi na kikosi cha timu hiyo bila ya kujua ni siku gani ataitumikia, hali hiyo imeonekana kumuumiza roho na kujikuta akisema kuwa endapo sakata lake na Simba litaendelea hivyo basi yupo tayari kukaa nje ya uwanja kwa msimu mzima.
Kessy ambaye alijiunga na Yanga hivi karibuni anashindwa kuitumikia timu hiyo kutokana na kile kinachodaiwa uongozi wa klabu hiyo haukuzingatia taratibu za usajili wakati ulipokuwa ukimsajili kutoka Simba.
Kutokana na hali hiyo uongozi wa Simba unataka Yanga ilipe Sh milioni 126, ili Kessy aweze kuitumikia vinginevyo hataitumikia klabu hiyo, jambo ambalo lilimfanya Kessy kwenda kuomba msaada kwa Chama cha Wachezaji wa Soka Tanzania (Sputanza), ili waweze kumsaidia kuhakikisha anapata kibali kutoka TFF, kitakachomwezesha kuitumikia timu hiyo mpya.
Kessy alisema mpaka sasa hakuna kilichofikiwa na kama hali hiyo itaendelea kama ilivyo sasa basi yupo tayari kukaa nje ya uwanja kwa msimu mzima.
“Suala langu bado linaendelea na mpaka sasa sijapata jibu lolote kutoka Sputanza hata hivyo kama itaendelea hivi basi nitasubiri mpaka litakapomalizika hata kama itakuwa ni kukaa nje msimu mzima mimi nitakaa.
“Kuhusu kiwango changu kushuka naamini hakitashuka kwa sababu nipo katika timu nzuri. Lakini pia  nipo chini ya kocha mzuri ambapo nitakuwa nafanya mazoezi kwa nguvu zangu zote mpaka hapo suala hili litakapomalizika,” alisema Kessy.

Post a Comment

 
Top