SIKU mbili tangu kikosi cha Simba kilipoisurubu Polisi Morogoro mabao 6-0, kocha mkuu wa timu hiyo, Mcameroon, Joseph Omog, amedai kuwa kikosi chake hicho hivi sasa kipo tayari kwa michuano ya Ligi Kuu Bara.

Mchezo huo wa kirafiki ulifanyika katika Uwanja wa Chuo cha Biblia kilichopo Bigwa mkoani Morogoro ambako timu hiyo imepiga kambi yake ya kujiandaa na ligi kuu inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi Agosti 20, mwaka huu.

Omog alisema kuwa kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji wake katika mchezo huo ni cha hali ya juu hivyo hata kama ligi kuu itaanza leo basi ana uhakika kuwa watafanya vizuri.

“Kwa sasa kikosi changu kipo vizuri na tayari kabisa kwa michuano ya ligi kuu kutokana na kiwango cha juu kilichoonyeshwa na wachezaji katika mechi yetu ya kirafiki dhidi ya Polisi Morogoro.

“Kila mchezaji aliyepata nafasi ya kucheza alionyesha kiwango kikubwa hali ambayo ilinifanya niamini hivyo,” alisema Omog.


“Kuhusu hatima ya wachezaji wa kimataifa wanaoendelea kujifua na kikosi chake, Omog alisema: “Wanafanya vizuri lakini kila kitu kitajulikana hivi karibuni nani atabaki na nani ataondoka, hivyo tuwe na subira.”

Omog alikabidhiwa mikoba ya kukinoa kikosi hicho hivi karibuni ambapo hivi sasa yupo katika harakati za kukisuka upya akisaidiana na Mganda, Jackson Mayanja ili kiweze kurudisha heshima yake iliyopotea kwa muda mrefu bila ya kushiriki michuano ya kimataifa lakini pia kunyakua ubingwa wa ligi hiyo.


Post a Comment

 
Top