KOCHA Bora wa msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara, Hans van Der Pluijm wa Yanga, amesema wataishangaza Medeama SC kwa kuifunga nyumbani kwao Ghana Jumanne ijayo kwenye mechi ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Pluijm, raia wa Uholanzi, alienda mbali kwa kusema, haoni sababu ya wao kushindwa kupata matokeo mazuri nchini Ghana wakati timu yake itakaporudiana na Medeama.
Mechi hiyo ya marudiano ya Kundi A ikiwa na kumbukumbu ya kutoka sare ya bao 1-1 hapa nchini.

Pluijm alisema kupoteza pointi mbili mechi ya nyumbani siyo sababu ya timu yake kushindwa kuifunga Medeama wakiwa kwenye uwanja wao wa nyumbani.

Pluijm alisema, siyo kazi rahisi kwao kuwafunga Medeama nyumbani kwao, lakini watapambana kwa pamoja kuanzia benchi la ufundi, viongozi na wachezaji kuhakikisha wanafanikisha hilo.

Aliongeza kuwa, tayari ameona mbinu na mifumo wanayotumia Medeama, hivyo amekiboresha kikosi chake ili kutimiza malengo, licha ya ugeni walionao kwenye michuano hiyo kwa hatua waliyofikia.


“Kadiri siku zinavyoenda benchi langu la ufundi na wachezaji kwa pamoja tunazidi kupata uzoefu wa michuano hii katika hatua hii tuliyoifikia ya mashindano haya.
“Hivyo, tunakwenda kurudiana na Medeama tukiwa tumepata uzoefu wa michuano hii katika nafasi hii ya hatua ya makundi, hivyo tutawavaa Medeama tofauti na watakavyotarajia, licha ya kumkosa Bossou (Vincent) mwenye adhabu ya kadi mbili za njano, nitamtumia Cannavaro (Nadir Haroub),” alisema Pluijm.

Kwa upande wake, nahodha wa Yanga, Cannavaro alisema: “Wanayanga na Watanzania wote wanatakiwa kutuombea, tunakwenda kupambana na timu bora siyo nyepesi.”

Post a Comment

 
Top