MCHEZAJI kiraka wa Yanga, Mnyarwanda, Mbuyu Twite, ameonyesha kuwa popote uwanjani anacheza kwa kiwango kilekile, baada ya kuchezeshwa nafasi tatu tofauti kwenye mechi za timu hiyo, hivi karibuni.
Twite ambaye hivi karibuni jina lake lilikuwa kwenye hatari ya kukatwa katika usajili wa timu hiyo, mpaka sasa ameshacheza mechi tatu za Yanga za kimataifa kwa dakika zote tisini mfululizo ambazo ni sawa na dakika 270.
Katika mchezo dhidi ya MO Bejaia ya Algeria, Twite alichezeshwa beki wa kulia baada ya Juma Abdul kuwa majeruhi, huku Hassan Kessy akizuiwa kucheza kutokana na uhamisho wake kutoka Simba kutokamilika.
Mchezo uliofuata wa michuano hiyo dhidi ya TP Mazembe, Twite alichezeshwa beki wa kushoto baada ya Oscar Joshua na Haji Mwinyi kuwa majeruhi.
Twite alidhihirisha kwamba yeye ni mtu muhimu kikosini hapo juzi Jumamosi walipocheza dhidi ya Medeama ambapo alitia fora kwa kucheza nafasi mbili tofauti.
Mnyarwanda huyo mwenye asili ya DR Congo, alianza kama kiungo mkabaji ambapo alicheza kwa dakika 78, lakini mara baada ya Oscar Joshua aliyekuwa akicheza beki wa kushoto kutolewa na nafasi yake kuchukuliwa na Haruna Niyonzima, Twite akacheza beki hiyo ya kushoto.
 Kocha wa Yanga, Hans van Der Pluijm, amemmwagia sifa mchezaji huyo akisema: “Kila ninapompatia majukumu ya kufanya uwanjani amekuwa akiyafanya kwa umakini mkubwa bila ya kuniangusha, hakika napongeza kwa hilo na nitaendelea kumtumia katika mechi zetu zijazo.”
 Kwa upande wake Twite alisema: “Hicho ni kipaji nilichopewa na Mungu, hivyo ninamshukuru Mungu kwa hilo, lakini pia najisikia faraja kwa kufanikiwa kuandika rekodi hiyo nikiwa na Yanga.”

Post a Comment

 
Top