MSHAMBULIAJI wa Medeama FC, Bernard Danso aliyefunga bao la kuchomoa la timu hiyo walipoumana na Yanga, ametamba kuwa ameshawasoma mabeki wa timu hiyo na lazima ataifunga tena Yanga katika mechi ya marudiano huko kwao Ghana.
Katika mchezo huo wa Kombe la Shirikisho Afrika uliopigwa Jumamosi iliyopita Uwanja wa Taifa, Yanga ndiyo ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia kwa Donald Ngoma dakika ya pili lakini halikudumu baada ya Danso kuchomoa bao hilo dakika ya 19 na kusababisha sare ya bao 1-1 yaliyoiacha mkiani Yanga katika Kundi A.
“Yanga ni timu nzuri lakini niliwasoma mabeki wao kwa dakika tano za mwanzo nikiwa uwanjani na kujua nifanye nini, tangu nakuja Tanzania nilipanga kuwa lazima nifunge na kweli imekuwa hivyo. Najua mechi ya nyumbani Ghana watanizuia sana lakini lazima nitawafunga tena.
“Lengo letu ni ushindi tu katika mechi zilizosalia na unaona Yanga ndiyo mechi inayofuata kwa hiyo ni lazima tuhakikishe ushindi kwenye mechi za mapema ingawa najua wataleta ushindani lakini sidhani kama wataweza kutuzuia,” alisema Danso aliyefunga mabao nane mpaka sasa kwenye Ligi Kuu ya Ghana.
Yanga iliyopo mkiani mwa Kundi A ikiwa na pointi moja baada ya mechi tatu inatarajia kurudiana na Medeama Jumanne inayokuja. Katika Kundi hilo, TP Mazembe ya DR Congo ndiyo kinara ikiwa na pointi saba, MO Bejaia (Algeria) ina tano kisha Medeama yenye mbili.



Post a Comment

 
Top