HAINAGA ushemeji, Yanga inakulaga Medeama, ndiyo wimbo utakaoimbwa na mashabiki wa Yanga leo Jumamosi wakati timu yao itakapokuwa ikipambana na Medeama ya Ghana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika kuhakikisha wanarejesha morali ya timu na kuwafariji mashabiki hao, Kocha Mkuu wa Yanga, Mholanzi, Hans van Der Pluijm ameapa kuwa ni lazima wawafunge Medeama ili mbele mambo yao yawe safi.

Yanga inacheza na Medeama mechi ya Kundi A ya Kombe la Shirikisho Afrika, ambayo itaonyeshwa moja kwa moja na Azam TV.

Yanga inahitaji ushindi ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kutinga nusu fainali ya michuano hiyo kwani ipo mkiani mwa kundi hilo ikiwa haina pointi huku TP Mazembe ikiwa kileleni na pointi sita.

Katika mchezo wake wa kwanza wa Kundi A, Yanga ikiwa ugenini ilifungwa na MO Bejaia ya Algeria bao 1-0, halafu ikafungwa tena bao 1-0 na TP Mazembe Juni 28, mwaka huu hapa nchini.

Pluijm alisema maandalizi makubwa aliyoyafanya ya wiki mbili yanatosha kabisa timu yake kupata ushindi kwenye mechi na Medeama.

Pluijm alisema tayari amewaona wapinzani wao kupitia video mbalimbali za mechi zao na kikubwa alichokiona Medeama wana fiziki ya kutosha, hivyo ni lazima aanzishe wachezaji wapambanaji.

Mholanzi huyo alisema, katika mechi hiyo anataka kuona kila nafasi watakayoipata ya kona, faulo na krosi wanaitumia vizuri kwa kufunga mabao ili kuhakikisha wanashinda mechi.

“Mechi yetu na Medeama ya kesho (leo) tutapambana kufa na kupona kuhakikisha tunapata ushindi ili saikolojia ya wachezaji wangu irejee kutokana na presha waliyonayo wakihitaji ushindi.

“Ninashukuru morali ya wachezaji wangu ipo juu na maandalizi niliyoyafanya yanatosha kutupa ushindi, najua siyo kazi rahisi, lakini tutapambana kuhakikisha tunawafunga Medeama.

“Kutokana na makosa ya safu yangu ya ushambuliaji kwenye mechi mbili tulizofungwa, nimeifanyia marekebisho kwa kuwapa mbinu mbalimbali washambuliaji wangu.

“Nimewapa mbinu za kucheza kona, faulo na krosi, hivyo nimewataka wachezaji wangu kutumia kila nafasi tutakayoipata kwa ajili ya kufunga bao,” alisema Pluijm.
Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, alisema:

“Sisi tupo vizuri na hatutaki kuwaangusha tena mashabiki wetu, waje uwanjani wapate furaha.”
Kwenye mazoezi yao ya jana jioni kwenye Uwanja wa Taifa, Dar, Medeama walizuia kupigwa picha huku wakionekana kuwa na hofu.

Kocha wa Medeama, Prince Owusu, alisema: “Naijua Yanga vizuri, tumekuja kupambana kwani wote bado tuna nafasi ya kuingia nusu fainali, sitarajii mchezo rahisi na wala Yanga isitarajie urahisi.”

Nahodha wa Medeama, Mohammed Tagoe, alisema wamekuja kushindana na kama wanabezwa ukweli utadhihirika uwanjani.  

Kutokana na mazoezi ya Yanga ya jana asubuhi kwenye Uwanja wa Boko Veterani, Dar, kikosi chao kinaweza kupangwa hivi: Deogratius Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, Oscar Joshua, Kelvin Yondani, Vincent Bossou, Mbuyu Twite, Simon Msuva, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma, Amissi Tambwe na Obrey Chirwa.

Post a Comment

 
Top