![]() |
Bukungu wa kwanza kulia |
BEKI wa zamani wa TP
Mazembe anayewania nafasi ya kusajiliwa Simba, Besala Janvier Bukungu amesema
anamjua vizuri straika wa Yanga, Donald Ngoma na mashabiki wa Wekundu wa
Msimbazi watulie kwani atamtuliza.
Pia
Bukungu alisema amepata taarifa kwamba Simba anayotaka kujiunga nayo
msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara ilifungwa mara mbili na Yanga, kisha akatikisa
kichwa.
Bukungu raia wa DR Congo amesikitishwa na
vipigo hivyo vya mabao 2-0, papo hapo akaliambia Championi Jumamosi kwamba: “Lazima tulipe kisasi na naahidi
mashabiki wa Simba hawatalia tena.”
Beki huyo anayemudu kucheza nafasi zote za
beki iwe kulia au katikati, alisema amepewa taarifa kwamba mara zote ambazo
Simba imefungwa na Yanga, mashabiki wake walikuwa wakiangua vilio, hivyo
amewaambia sasa basi imetosha.
Bukungu mrefu na mwenye mwili mkubwa alisema
anaamini kama mambo yakienda sawa na akasajiliwa na Simba, hawatakubali
kufungwa tena na Yanga.
Ngoma |
Beki huyo tayari amejiunga na Simba na kuanza
mazoezi ya pamoja chini ya kocha mpya raia wa Cameroon, Joseph Omog aliyetua
wiki iliyopita na kusaini mkataba wa miaka miwili ya kukinoa kikosi hicho.
“Wanasimba wajiandae kufurahia kwenye msimu
ujao na siyo vilio kila walipokuwa wanakutana na Yanga kisha kufungwa,
nitashirikiana na wenzangu kuwapa furaha mashabiki wa Simba,” alisema Bukungu.
Bukungu ambaye aliwahi kuichezea timu ya taifa
ya DR Congo na klabu kubwa za TP Mazembe na Esperance ya Tunisia, alisema:
“Nimesikitishwa na taarifa za Yanga kuifunga Simba mara zote walizokutana
kwenye ligi kuu, kiukweli nimeumizwa nazo na niwaahidi Wanasimba kuwa ni lazima
tulipe kisasi kwa staili yoyote.
“Hakuna kisichoshindikana kwangu, mimi kama
beki nitatimiza wajibu wangu wa kutokubali kuruhusu bao liingie golini kwetu,
hivyo nitapambana kuhakikisha tunawafunga Yanga kila tutakapokutana nao,”
alisema Bukungu.
“Niwaambie tu mashabiki wa Simba kuhusu
straika wa Yanga anaitwa Ngoma, namjua na nimewahi kukabana naye katika mechi
za timu za taifa, yeye akiwa Zimbabwe mimi DR Congo.
“Siyo mtu anayetisha sana, ila inatakiwa
umakini kumzuia na mimi nitaifanya hiyo kazi kama mambo yakienda vizuri halafu
utaona kama Simba itafungwa tena na Yanga,” alisema Bukungu.
Naye kiungo mshambuliaji raia wa DR Congo,
Mousa Ndusha anayewania kusajiliwa Simba, alisema: “Ni bora tufungwe na Azam FC
ambayo naamini wanacheza soka safi na la kuvutia lakini siyo Yanga.
“Yanga niliwaona wakicheza na TP Mazembe, siyo
timu ya kuiogopa na inafungika.”
Post a Comment