SASA ni asilimia zaidi ya 80 mshambuliaji Kipre Herman Tchetche hatarejea nchini kuitumikia Azam FC kwa kuwa amegoma kurejea.

Tchetche, raia wa Ivory Coast, inaelezwa yuko nyumbani kwao ambako ameamua kubaki na kukataa kujiunga na kambi ya Azam FC hali ambayo imezua hofu na kuunganisha kwamba mabingwa wa Tanzania, Yanga wamemficha.

Mmoja wa viongozi wa Yanga ambaye hakutaka kutajwa jina, amesema hivi: “Kweli Kipre ni mchezaji bora, kama tukimhitaji basi tunajua cha kufanya. Ila si wakati mwafaka kulizungumzia, kama hajarudi Azam, hilo ni yeye na timu yake.”

Hata hivyo, Azam FC wanaonekana kutokuwa na hofu kwa kuwa mchezaji huyo amebakiza mkataba wa mwaka mmoja na timu hiyo ya Chamazi na kocha mpya, Zeben Hernandez amekuwa akisisitiza kwamba anamhitaji.

“Kuna hofu kuwa kuna timu inamrubuni Kipre, uongozi wa Azam FC uko imara kwa kuwa ana mkataba wa mwaka mmoja, watajisumbua tu,” kilieleza chanzo kutoka ndani ya Azam.

Rafiki wa karibu wa Kipre ameliambia gazeti hili kuwa Tchetche alizungumza na mmoja wa mabosi wa Azam FC na kusema ameshindwa kuja kwa kuwa aliuziwa nyumba kwao Ivory Coast lakini kuna harufu ya utapeli.

“Baada ya juhudi za kumpata kwa zaidi ya wiki, juzi alipatikana akazungumza na mmoja wa mabosi na kusema anachelewa kwa kuwa alitapeliwa katika mauzo ya nyumba, hivyo hadi alimalize suala hilo na hatujui ni lini,” kilifafanua zaidi chanzo.

Tayari Azam FC imeanza maandalizi ya msimu mpya chini ya Hernandez na jopo lake na kocha huyo ameusisitiza uongozi kufanya juu chini kumrejesha kundini.

Kuhusu Yanga kumhitaji, wakati fulani Kocha Hans van Der Pluijm aliwahi kusema wazi kwamba angependa kuwa naye katika kikosi chake.

Yanga kushindwa kuonyesha cheche katika michuano ya kimataifa hasa katika safu ya ushambuliaji chini ya Donald Ngoma, Amissi Tambwe na Obey Chirwa, inaweza kuchangia Yanga kufanya juu chini kumpata kwa kuwa ina michuano ya Ligi ya Mabingwa, msimu ujao.

Alipoulizwa kuhusiana na hilo jana, Msemaji wa Azam FC, Jaffar Iddi alisisitiza hivi: “Kipre ana mkataba na Azam, kama kuna timu inamhitaji inakaribishwa na uongozi. Suala la amefika au atafika lini, litafuata baadaye.”

Taarifa nyingine zinaeleza, Kipre ameingia katika hali ya kutoelewana na mmoja wa viongozi wa Azam FC, hali ambayo inamfanya aone Yanga ni sehemu sahihi kwenda.

Kama ataendelea kuchelewa, Azam FC imesisitiza itamwadhibu na kama anataka kuuzwa, vema akaiambia klabu. Kocha Hernandez licha ya kumtaka, naye amechukua tahadhari kuanza kutafuta mshambuliaji mpya wa uhakika hasa iwapo, ishu ya kumrejesha itakwama kwa asilimia 100.

Tayari wachezaji kadhaa wa kimataifa wamekuwa wakipishana kufanya majaribio katika kikosi hicho.

Post a Comment

 
Top