UONGOZI wa Simba umethibitisha kupokea barua kutoka Yanga ya kuomba barua ya kumuidhinisha beki wao wa pembeni, Hassan Kessy kuichezea timu hiyo kwenye msimu ujao wa Ligi Kuu Bara na Kombe la Shirikisho Afrika.
Beki huyo, hivi karibuni alizua mijadala kwenye timu hizo kongwe wakati moja ikisema imepeleka barua ya kuomba kuidhinishwa huku nyingine ya Simba ikikana kupokea barua hiyo.
Kessy hadi hivi sasa hivi amekosa michezo miwili ya Kombe la Shirikisho Afrika ambayo ni dhidi ya MO Bejaia na TP Mazembe kutokana na kutopata barua ya kuidhinishwa kutoka Simba.
Kanuni za Shirikisho la Soka Afrika (Caf) zinaitaka Simba kutoa barua hiyo ndipo Yanga imtumie Kessy.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Rais wa Simba, Evans Aveva, Jumatano wiki hii walipokea barua kutoka Yanga wakiomba barua ya kumuidhinisha beki huyo ili wamtumie kwenye michuano ya kimataifa.
Aveva alisema, suala hilo limefikia kwenye hatua nzuri za kumuidhinisha Kessy ili aichezee Yanga katika Kombe la Shirikisho la Afrika.
Aliongeza kuwa, uamuzi wa kumuachia beki huyo, utaenda sambamba na kikao cha Kamati ya Utendaji ya Simba itakapokutana na kulijadili suala hilo kabla ya kuipatia Yanga barua ya kumuidhinisha.
“Nikuhakikishie tu, suala la Kessy limefikia pazuri kwa maana ya kumruhusu kuichezea Yanga kwa kumpatia barua ya kumuidhinisha kuichezea Yanga kwenye michuano ya kimataifa.
“Sidhani kama ni vizuri kumzuia Kessy, kikubwa tulipokea barua kutoka Yanga ikiomba tuwapatie barua ya kumuidhinisha Kessy aichezee timu yake hiyo mpya.
“Hivyo suala hilo siyo la kwangu pekee linahusisha kamati nzima ya utendaji, kamati imepanga kukutana hivi karibuni kwa ajili ya kujadiliana suala hilo na kufikia muafaka mzuri,’ alisema Aveva.
Aidha, alipotafutwa Katibu Msaidizi wa Chama cha Wachezaji wa Soka Tanzania (Sputanza), Abeid Kasabalala kuzungumzia suala hilo, alisema: “Tumewasilisha barua TFF ya kuomba kutoa kibali cha kumruhusu Kessy kuanza kucheza, pia Simba na Yanga kukaa pamoja kulimaliza tatizo hilo na siyo kutunishiana misuli.”

Post a Comment

 
Top