MSHAMBULIAJI anayewaniwa na Simba SC, Mrundi Laudit Mavugo inadaiwa ametimkia Ufaransa kufanya mipango ya kujiunga na klabu ya Tours ya Ligi Daraja la Pili, maarufu kama Ligue 2.
Na Mavugo anakwenda Ufaransa wakati tayari Simba SC wamesema wamekwishaingia Mkataba na mchezaji huyo kuanza kuwatumikia kuanzia msimu ujao.
Wakala Dennis Kadito aliyewahi kumsimamia wakati fulani mchezaji huyo apate timu Ulaya amesema kwamba amesikia taarifa za Mavugo kwenda Ufaransa, lakini hahusiki na hajui lolote.
"Nimesikia tu, kwa nini msimuulize yeye mwenyewe,"alisema Kadito ambaye mwaka jana alijaribu kumleta Simba SC mchezaji huyo.
Lakini mchezaji mwenzake Mavugo katika timu ya taifa ya Burundi ametihibitishia leo kwamba mwana Int'hamba Murugamba mwenzake huyo amekwenda Ufaransa.
Alisema siku Mavugo anaondoka alikutana naye Uwanja wa Ndege wa Bujumbura akiwa na familia yake ikimuaga kwa ajili ya safari ya kuelekea nchini humo.
"Nilikutana naye Uwanja wa Ndege wa Burundi, akiwa na familia yake wakimuanga, kwani amepata ofa ya kwenda Ufaransa kufanya majaribio katika timu ya Tours inayoshiriki Ligi Daraja la Pili," alisema rafiki huyo.
Bado haijulikani Simba SC itachukua gani kwa Mavugo, kwa kuwa makubaliano yao na mchezaji huyo bado yanafanywa siri ili kuepuka vikwazo kutoka klabu yake, Vital'O.
CHANZO: BIN ZUBEIRY

Post a Comment

 
Top