MUNGU akiamua
huifanya ngumu ionekane nyepesi na laini yaweza kuwa yabisi. Ni yeye
aliye juu hubatilisha mipango ya binadamu kwa namna anavyotaka. Ndiyo
maana ikasemwa jitihada hazishindi kudura.
Ni kwa ukuu wa
Mungu, Bikira Maria, mwanamke ambaye alikuwa hajamjua mwanaume, alibeba
mimba ambayo ilimleta duniani Yesu Kristo (Isa bin Mariam).
Hapa ngoja
niweke kituo, kisha nikuhoji, ni kipi hasa kinachoweza kukufanya
ukimbilie kutoa mimba? Unamjua aliye tumboni mwako amepangwa na Mungu
awe nani hapa duniani?
Wewe mwanamke
unayenyonga kichanga, ni kwa nini unawahi kukata tamaa mapema na
kupitisha hukumu kuwa huwezi kumlea mwanao? Je, unatambua ni sahani gani
ambayo Mungu amempa aje nayo hapa duniani?
Umewahi
kujiuliza, hivi kama Mark Zuckerberg angetolewa akiwa mimba na mama yake
wakati huo, ni nani angeleta mapinduzi ya matumizi ya mtandao kupitia
Facebook?
Vipi Bill Gates
na Microsoft yake, angewezaje kuyafanya maisha yetu ya kila siku kikazi
kuwa rahisi kama mama yake angemnyonga akiwa kichanga?
Ni kwa kufikia
hoja hiyo ndipo unaweza kuona kuwa wapo watu wengi ambao walimaanishwa
kuifanya dunia kama peponi lakini safari yao ilibaki njiani kwa sababu
wazazi wao hawakuwapa nafasi ya kuishi.
Ngoja nikwambie
ndugu yangu, fursa ya kuishi anaitoa Mungu na ni yeye mwenyewe
huyakatisha maisha ya mja wake kwa wakati na namna atakavyo. Juhudi
zozote za kukatisha maisha ya mtu ni kuingilia mamlaka ya Muumba!
Mimba
inapoingia tumboni, hebu hakikisha unaitunza, maana Mungu ametoa fursa
kwa mja wake mwingine kuja duniani. Harakati zako za kwenda kwa
madaktari kuichoropoa, kwanza unashindana na mamlaka ya Mungu, pili
unapiga teke sahani la almasi.
Je, hupendi
kuwa mzazi wa Lionel Messi wa soka? Hutajisikia fahari endapo Steven
Curry wa kikapu NBA atakuwa mwanao? Huwezi kufikia hatua hiyo muhimu ya
heshima kama hutatii amri ya Mungu, anapoelekeza kiumbe chake ndani ya
tumbo lako.
Mwanamke
anaweza kutoa mimba kadhaa, kumbe hizo ndizo za wanasayansi wengine kama
Neil Armstrong na Buzz Aldrin, waliotangulia kufika mwezini na kufanya
ugunduzi mkubwa.
Ungependa
mwanao awe mgunduzi wa kihistoria kama Thomas Edison, aliyetengeneza kwa
mara ya kwanza taa za umeme, vifaa vya kurekodia sauti na kamera za
video, lakini wakati watoto wenye akili kubwa umewanyima fursa ya
kuishi.
Lea mimba kwa
unyenyekevu wa hali ya juu ikiwa unatamani kuwa na watoto wenye sifa
bora kama The Wright brothers, yaani Orville na Wilbur Wright,
waliotengeneza na kurusha ndege kwa mara ya kwanza, hivyo kuwa
waanzilishi wa usafiri huo wa anga.
Amini kuwa
Mungu anapoleta kiumbe chake, anakuwa analeta na sahani yake. Usiogope
changamoto za maisha. Endapo utazivumilia si ajabu ukamleta duniani
Nikola Tesla, aliyegundua mfumo wa kisasa wa umeme au mwanasayansi Marie
Curie ambaye ni mwanamke wa kwanza duniani kutunukiwa Tuzo ya Nobel.
Kuja kuitwa
mama wa mfalme, zipo gharama ambazo hutakiwi kuzikimbia. Nyingine ndiyo
kama hizo kwamba uwe tayari kubeba mimba katika kipindi ambacho unaona
kabisa maisha yako ni magumu.
Mungu ana
kawaida ya kuruhusu majaribu yakufike ili yakikuzidi nguvu upotoke. Na
mpotokaji anakuwa amechagua njia ya Shetani. Mungu huwapa akili nzuri
waja wake pamoja na utashi unaojitosheleza. Unapokosea kwa sababu yoyote
ile, maana yake umeshindwa kutumia akili yako ipasavyo.
Muhimu
kuzingatia ni kuwa unapopotoka, unakuwa umeshika njia ya Shetani. Mungu
aliyekuumba hutaka ubaki kwenye mstari wake hata unapokuwa kwenye wakati
mgumu kiasi gani. Muelekee yeye nyakati zote, kuwa na imani isiyoyumba.
Ni kwa imani
yako, ndipo unaweza kumleta duniani, Sandford Fleming ambye ni mgunduzi
wa majira, mwanzilishi wa stempu za barua, vilevile kiungo muhimu wa
uwekwaji wa njia za reli duniani. Usitoe mimba, pengine ukawa mama wa
rais au waziri mkuu.
CRISTIANO RONALDO ANGETOLEWA AKIWA MIMBA
Dolores Aveiro
ni mama wa staa wa soka duniani, Cristiano Ronaldo, anaitwa mama wa
stadi huyo wa mpira wa miguu kwa kudura za Mungu. Matunda anayokula
ku[itia mwanaye hakika hakuyastahili. Maana anakula raha alizojaribu
kuzihujumu.
Kama mipango ya
binadamu peke yake ingekuwa inatosha kutimiza mambo na maazimio,
Dolores asingeweza kuwa mwanamke maarufu duniani. Asingeitwa mama wa
kijana gwiji wa soka duniani, anayeichezea Klabu ya Real Madrid na Timu
ya Taifa ya Ureno.
Dolores
hakumtaka Ronaldo wakati ikiwa mimba lakini sasa hivi anatamba huku na
huko kwamba yeye ndiye mama mzaa nyota. Mungu alimlinda Ronaldo.
Mama huyo,
alikusudia hasa kukatisha maisha ya Ronaldo akiwa bado mimba, kwani hata
madaktari walipomshauri asifanye hivyo, alitumia mpaka njia za
kienyeji.
MAMA RONALDO ANAKIRI
Dolores
ameandika kitabu na kukiita kwa Lugha ya Kireno, Mae Coragem (Mother
Courage), maana yake ikiwa ni Ujasiri wa Mama. Ndani ya kitabu hicho
Dolores anasema: “Nililenga kutoa mimba ya Ronaldo. Nilitumia njia
nyingi bila mafanikio.”
Anaongeza:
“Madaktari waligoma kunisaidia kutoa mimba, uamuzi uliofuata baada ya
hapo ikawa ni kunywa pombe kali ili kutoa mimba. Lakini sikupata matokeo
niliyohitaji.
“Nilitumia kila njia nikashindwa. Sikutaka kumzaa Ronaldo. Sikujua kama atakuja kuwa huyu anayenifanya nijivunie kuwa mama.”
RONALDO AMRUDI MAMA YAKE
Ronaldo anajua
hila za mama yake, na siku moja alimrudi, akamwambia: “Mama angalia,
ulitaka kunitoa nikiwa mimba na sasa mimi ndiye kinara wa nyumba yetu.
Unanitegemea na familia yetu yote inanitazama mimi.
“Tazama jinsi
ambavyo dunia inanitazama. Naitwa mchezaji mkubwa duniani. Kila klabu
kubwa ya soka duniani ingependa kupata huduma yangu. Unadhani hii ni
fahari yangu peke yangu? Inakuhusu na wewe mama yangu. Unapaswa
kujivunia sana kuwa na mtoto kama mimi.
“Hata hivyo,
usingenipata kama ungefanikiwa. Unaweza kuona somo unaloweza kutoa kwa
wanawake wengine kuhakikisha wanatunza mimba na kuwalea watoto wao ili
waje kujivunia uwepo wao. Pengine wakawa watoto wenye umashuhuri mkubwa
duniani.”
Mume wa
Dolores, Dinis Averio ambaye ni baba wa Ronaldo, alishatangulia mbele za
haki kwa maradhi ya kuharibika kwa ini, ikiwa ni matokeo ya kuathirika
na unywaji pombe kupita kiasi.
Hata hivyo,
Ronaldo aliijua siri hiyo tangu akiwa mdogo lakini amekuwa akiitunza
bila kuitamka popote mpaka pale mama yake alipoamua kuvunja ukimya kwa
kuandika kitabu.
NINI SHABAHA YA KUANDIKA KITABU?
Kwa mujibu wa
Dolares, shabaha yake ni kuwafanya wanawake wengine waone matokeo yake
ili wajifunze kwamba unaweza kutoa mimba na kujidanganya kuwa ni salama
kumbe umepoteza mkombozi.
“Ningefanikiwa
kumtoa Cristiano akiwa mimba, maana yake nisingekuwa mama mwenye thamani
kubwa kama nilivyo sasa. Nilikubali kumwacha Cristiano akue tumboni
kwangu baada ya kushindwa kumtoa. Nilisema basi tu acha nizae lakini
siyo kwa mapenzi yangu.
“Wakati
mwingine mpaka huwa nashangaa kila nikikumbuka nilivyokuwa napigania
kuitoa mimba ambayo ndiyo imemleta Cristiano duniani. Nikimtazama
Cristiano alivyo mkubwa na anavyowika, najiona kabisa kuwa nilitaka
kufanya jambo baya na nilikaribia kukatisha maisha ya nyota ya dunia.
“Ananisuta
lakini najivunia, maana simuoni mama ambaye asingependa Cristiano awe
mtoto wake. Tumboni kwangu ameishi, nilimzaa na kumlea mimi mwenyewe.
Ndiyo maana nasema ananisuta lakini najiona mama mwenye fahari kubwa
kupitia mwanangu Cristiano,” anasema Dolares.
Anaendelea:
“Ona sasa, nimeandika kitabu na kuuza nakala nyingi kwa sababu
nimemzungumzia mtoto wangu ambaye ni maarufu sana duniani. Nimepata
mafanikio makubwa, nimeingiza fedha nyingi. Nafaidika sana kupitia kuwa
mama wa Cristiano.
“Upande
mwingine, mimi sina wasiwasi juu ya maisha yangu. Cristiano ananiwezesha
kwa kila ninachohitaji. Nikipita barabarani naheshimika. Serikali ya
Ureno inaniheshimu. Nikiwa Hispania au popote, hata Uingereza
naheshimika.
“Nafahamika
mimi ni mama wa Cristiano. Ni faida kubwa sana hii. Daima najivunia kuwa
mama wa Cristiano. Nampenda sana Cristiano, namshukuru Mungu kwa kuzuia
mpango wangu kutoa mimba yake.”
ANAFAIDI UTAJIRI WA MWANAYE
Kwa sasa
Ronaldo anashikilia rekodi ya kuwa mmoja wa wanamichezo wanaoingiza
fedha nyingi sana kupitia mshahara na mikataba ya matangazo.
Anatumia gari
apendalo na anaishi kwa ufahari mkubwa. Hayo ndiyo matokeo ya Mungu
kumlinda Ronaldo mpaka kufikia mafanikio yaliyopo kwa sasa. Na hiyo ni
sawa tu na ile bahati ya mtende kuotea jangwani.
WAPO WENYE JUHUDI KUBWA ZA KUUA
Mtu anafanya jaribio la kwanza, mimba haitoki, anarudia tena na tena. Hiyo ni dhamira ya hali ya juu.
Mwingine anafikisha mimba 10 mpaka 20, zote katoa. Kila mwaka anaweka rekodi ya kuchoropoa tatu mpaka nne.
Unaweza
kujiuliza kuna nini ambacho mtu anakuwa anakitafuta. Hawezi kuwaza ni
wanasayansi wangapi, idadi gani ya wachumi, wanasiasa wakombozi wa nchi,
madaktari wenye karama kubwa, waandishi wamulika nchi na kadhalika.
Unakuta mtu anafanya majaribio yote hayo, kisha analaumu kuwa katika uzao wake hajapata mtu mwenye kipaji maalum.
Kila mwanamke
atambue kuwa ndani ya tumbo lake kuna tunu kubwa mno. Ni jukumu lake
kuitunza. Njia pekee ya utunzaji wa tunu hiyo ni kukilinda kiumbe
kinachoingia ndani yake. Zingatia uaminifu!
Kwa mfano mmoja
tu wa mama yake Ronaldo, tafakari ni idadi gani ya akina Ronaldo
wanapotea? Ndiyo sababu mimi huwa nawaambia watu kuwa Mtanzania
aliyetakiwa kuchukua tuzo ya Mchezaji Bora wa Dunia (ballon d’or)
kumzidi Messi, pengine alitolewa akiwa mimba au alinyongwa akiwa
kichanga.
Mwanamke
Mtanzania tishio wa tenisi duniani, mwenye viwango kuliko Serena
William, inawezekana naye alinyimwa fursa ya kuishi na wazazi wake, kwa
ama kutolewa akiwa mimba au alinyongwa akiwa kichanga au hata alitupwa
chooni.
Chukua hii;
Kila siku kataa kuupofusha ubongo wako kwa sababu ya upeo wa mboni zako.
Kila uamuzi unaofanya hakikisha unatazama juu na mbali kabisa.
Changamoto za leo zisikunyime matunda ya kesho.
Hebu nikuombe
tuzungumze biashara nzuri na rahisi mno lakini yenye mtaji mkubwa na
faida yake inaweza kukufanya ufurahie maisha yako yote. Ukashangaa kila
siku unatabasamu, ukitembea unajivuna na watu wanakuheshimu bila shaka.
Kimsingi ni
biashara ambayo hata siku moja haiwezi kukupa majuto. Nakuhakikishia
pasipokuwa na chembe ya shaka kwamba haitatokea ikakufanya ujilaumu
kuifanya.
Naomba uniamini
mimi, biashara yenyewe ni uwekezaji kwa mtoto. Wekeza kwa mwanao kisha
utaona jinsi maisha yanavyoweza kubadilika kwa kasi.
Weka mipango safi kwa ajili ya mtoto wako na hakikisha unamwita jina zuri kisha umjenge katika misingi iliyo bora.
Usiwe mbinafsi, mpe anachohitaji kama kipo ndani ya uwezo wako. Mwoneshe upendo mpaka yeye mwenyewe akiri kwamba anapendwa.
Watoto ni wakoseaji mara nyingi, siyo yeye ni utoto. Muonye na umsahihishe kwa upendo. Mkaripie na umuadhibu kwa upendo.
Kuwa mtu wa
shukurani kila siku. Usimkufuru Mungu. Amini kuwa kwa Muumba kuna neema
nyingi nje ya matarajio pamoja na maombi yako. Tambua kwamba aliyekuumba
anakupenda kuliko unavyojipenda wewe mwenyewe.
Tukubaliane
sasa; Endapo utapata mimba, furahi na useme kuwa hayo ni mafanikio.
Usithubutu kusema kuwa imekuja kinyume na matarajio.
Pengine mimba unayosema imekuja kinyume na mipango, ndiye zawadi ya ukombozi. Ipokee na uithamini. Nakuhakikishia hutajuta.
Kuna siku ngumu
inakuja, ambayo wengi watashindwa kujibu maswali ya Muumba na malaika
wake. Siku tamu kwa watu wema na ngumu kwa waovu. Inaitwa siku ya
mwisho.
Siku hiyo
hukumu itatolewa. Na ikifika, wapo marais, wanasiasa wakubwa,
wanasayansi waliomaanishwa kuja kuikomboa dunia, viongozi wa kidini na
kadhalika, watasimamishwa kwenye uwanja wa hukumu, kisha kutangazwa kuwa
ni mashujaa walionyimwa fursa ya kuishi na wazazi wao.
Tuendelee kukumbushana. Tunaweza kujenga kizazi kizuri kwa faida ya leo na kesho.
mwandishi: Luqman Maloto
Post a Comment