VIJANA wa kihuni waliokuwa wamevaa nguo maalum za kuficha
sehemu kubwa ya sura zao, Jumatano iliyopita walifanya tukio la uvamizi katika
nyumba ya mshambuliaji wa Manchester United, Wayne Rooney.
Wahuni hao walivamia katika jumba hilo lenye thamani ya pauni
milioni 6 wakati Rooney na familia yake walipokuwa kwenye Uwanja wa Old
Trafford kwa ajili ya mechi maalum ya kirafiki ya man United dhidi ya Everton.
Polisi walilazimika kufika haraka katika jumba hilo lililopo
mitaa ya Cheshire baada ya alamu iliyopo ndani ya nyumba hiyo kuwaka na kutoa
mlio wa hatari, hali ambayo ilithibitishwa na majirani wa nyumba hiyo ambayo
Rooney anaishi na mkewe, Coleen na watoto wao watatu, Kai, Klay na Kit.
Polisi wakiwa ndani ya helikopta na magari kadhaa, walifika
nyumbani hapo wakiwa na silaha pamoja na mbwa kwa ajili ya uchunguzi ambapo
inaelezwa wahuni hao hawakufanikiwa kuingia ndani ya nyumba hiyo.
Jinarani mmoja akielezea tukio hilo alisema: “Wayne ana
ulinzi mzuri sana kwa Coleen na watoto wake hasa pindi anapokuwa mbali. Kilichotokea
ilikuwa kama filamu baada ya alamu kuwaka kutokana na wahuni hao kuvamia.
“Polisi walikuwa wengi na walizunguka eneo hili ndani ya muda
mfupi.”
Hakuna mtu aliyekamatwa katika tukio hilo lakini Rooney
alijulishwa kilichotokea muda mfupi baada ya mchezo wa Everton kumalizika.
Tukio hilo lilitokea kati ya saa 2.30 na 2.45 usiku, wakati
Rooney alipokuwa pamoja na familia yake katika mchezo huo.




Post a Comment