KAMPUNI ya Wachina ya Beijing Construction and Engeenering Group leo imeukabidhi rasmi Uwanja wa Uhuru kwa Waziri wa Habari Sanaa Utamaduni na Michezo, Nape Nnauye kwa niaba ya Serikali baada ya kukamilika kwa marekebisho yake yaliyoanza miaka mitatu iliyopita.

Marekebisho hayo yaliyoanza mwaka 2013 yameigharimu Serikali shilingi 12 Bilioni na sasa uwanja huo utakuwa na uwezo wa kuingiza mashabiki 23,000 walioketi.

"Niwaombe wadau waendelee kuiunga mkono Serikali kwa kuwekeza kwenye michezo ili kuifanya nchi yetu kufanya vizuri zaidi kimataifa," alisema Nape.

Kwa upande wake Katibu mkuu wa Wizara ya Habari Elisante Ole Gabriel alimuhakikishia Waziri Nape kuwa miundo mbinu ya uwanja huyo italindwa ili iendelee kudumu zaidi kama matakwa ya Serikali.

Katika hatua nyingine Katibu mkuu huyo amepiga marufuku uwanja huo kuitwa 'Shamba la Bibi' kutokana na historia kubwa ulionao kwa Taifa hili tangu nchi ilipopata Uhuru.


Post a Comment

 
Top