SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limesema endapo Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji ataendelea na msimamo wake wa kutaka wanachama watatu wa klabu hiyo kufutwa uanachama wao, basi anaweza kufungiwa si chini ya miaka 10.

Juni 6, mwaka huu, Klabu ya Yanga ilifanya mkutano wa dharura ambapo Manji aliwafuta uanachama wanachama watatu wa klabu hiyo ambao ni Ayoub Nyenzi, Salum Mkemi na Hashimu Abdallah, kutokana na sababu zilizoelezwa kutaka kuihujumu Yanga.

Baada ya wanachama hao kufutwa uanachama, wakaamua kupeleka malalamiko yao TFF wakidai mwenyekiti wao alikiuka katiba ya klabu hiyo.

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya TFF, zinasema kuwa wanachama hao ambao pia ni Wajumbe wa Kamati ya Utendaji Yanga, watarudishiwa uanachama wao na kuendelea na majukumu yao kama kawaida.

“Kila kitu kipo wazi, Nyenzi na wenzake watarudishiwa uanachama wao na kurudi kwenye vituo vyao vya kazi kama kawaida na endapo Manji atashikilia msimamo wake wa awali, basi atafikishwa katika Kamati ya Maadili ya TFF na adhabu yake ni kifungo si chini ya miaka 10,” kilisema chanzo hicho.

Wakati huohuo, Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas, amesema: “Kamati ya Maadili ya TFF inatarajiwa kukaa Jumapili hii kuijadili ile barua iliyowasilishwa na wanachama wa Yanga waliofutwa uanachama.”
Chanzo: Championi

Post a Comment

 
Top