WAKATI Barcelona ikitarajiwa kuivaa Liverpool, leo Jumamosi, straika wa Barcelona, Luis Suarez amesema anafurahia kuona anakutana na rafiki zake aliocheza nao muda mrefu.

Timu hizo zinakutana kwenye Uwanja wa Wembley ikiwa ni michuano ya International Champions Cup ambayo ni mwendelezo wa mechi za kujiandaa na msimu mpya, hiyo itakuwa mara ya kwanza kwa Suarez kukutana dhidi ya timu yake hiyo ya zamani tangu alipoondoka mwaka 2014.

Kwa sasa Suarez ni mchezaji tegemeo kwenye kikosi cha Barcelona, heshima aliyoitengeneza akiwa Liverpool ya kufunga mabao 82 katika mechi 133 ilimfanya kuwa kipenzi cha wengi kikosini hapo mpaka sasa.

"Ni wakati mzuri kwa mashabiki. Nina marafiki wengi pale, nafikiri ni jambo zuri kukutana nao na kucheza dhidi yao,” alisema Suarez na kuendelea:

"Kwa mchezaji unapocheza mbele ya mashabiki 90,000 ni ndoto kuwa kweli. Mashabiki wa Liverpool ni watu wa kipekee duniani na ninadhani wana hamu na mchezo huo pia.”
“Kila mtu anajua jinsi Liverpool ilivyo muhimu katika maisha yangu binafsi na ya soka. Mtoto wangu wa pili nilimpata nikiwa hapo na ninakumbuka kuwa na nyakati nzuri sana hapo.”

Post a Comment

 
Top