LIGI Kuu ya England ‘Premier League’ inaendelea wikiendi hii ambapo vigogo wote watakuwa uwanjani kutafuta ushindi huku gumzo ikiwa ni mchezo wa Tottenham dhidi ya Liverpool.

Mchezo huo ambao unatarajiwa kuchezwa leo Jumamosi kwenye Uwanja wa White Hart Lane, utakuwa wa kwanza kabisa kabla ya mechi nyingine kuchezwa jioni, huku ikikumbukwa kuwa timu hizo zote zipo katika ushindani mkali.


Tottenham maarufu kwa jina la Spurs ina pointi nne katika michezo miwili wakati wapinzani wao, Liverpool wana pointi tatu na wanahitaji ushindi kwa kuwa katika mchezo uliopita walifungwa, hivyo pointi tatu za leo zinaweza kuamsha furaha ya timu hiyo ambayo ilipotea wikiendi iliyopita.

Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp alichukizwa na wachezaji wake kutofuata maelekezo yake katika mchezo uliopita na kuahidi kuwa atarekebisha makosa na hivyo mchezo wa leo ndiyo unatakiwa kuthibitisha hilo japokuwa Spurs ni moja ya timu ngumu.

Wakubwa wengine wa ligi hiyo, Manchester United watakuwa ugenini kwenye Uwanja wa The KC kuwa wageni wa Hull City, wakati wakali wa London, Chelsea watakuwa nyumbani kukipiga na Burnley kwenye Uwanja wa Stamford.

Watford watakuwa nyumbani kuikaribisha Arsenal huku mabingwa watetezi Leicester City wakiwa wenyeji wa Swansea City.

Vijana wa Pep Guardiola, Manchester City nao watakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Etihad kuwavaa West Ham.

Post a Comment

 
Top