MKUU wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Jerry Muro, ametamka kuwa jana Ijumaa ndiyo alianza kazi rasmi kwenye timu hiyo.
Kauli hiyo, ameitoa ikiwa ni siku chache tangu mwenyekiti wa timu hiyo, Yusuf Manji kuagiza Muro aanze kazi mara baada ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutangaza kumfungia mwaka mmoja.
TFF ilimfungia Muro hivi karibuni kufuatia madai ya kulishambulia shirikisho hilo, hivyo atatakiwa kukaa kwa kipindi hicho.
Muro alisema ameanza kazi rasmi baada ya kumaliza likizo yake Agosti 2, mwaka huu na jana aliripoti ofisini kwa mara ya kwanza.
Muro alisema, taarifa za kufungiwa amezisikia lakini hana nakala ya barua ya hukumu yake, hivyo ameiomba TFF kumpelekea barua hiyo kwa ajili ya kuipitia na kujua sababu iliyowafanya wamfungie.
Aliongeza kuwa, mara baada ya kupokea nakala hiyo, haraka atakutana na viongozi wake kwa ajili ya kupitia kanuni na sheria zilizotumika yeye kufungiwa mwaka mmoja.
“Naomba nichukue nafasi hii kuwatangazia Wanayanga kuwa, mimi leo (jana) ndiyo nimeanza kazi rasmi Yanga na niliripoti kazini tangu Agosti 2, mwaka huu.
“Nimefika hapa ofisini na kupata taarifa za mimi kufungiwa, sikatai kufungiwa lakini kikubwa ninachoomba ni kupatiwa nakala ya barua ya hukumu kutoka TFF na badala ya hapo ndiyo mengine yafuate.
“Mara baada ya kupata nakala hiyo, kikubwa ninataka kujua sababu ya mimi kufungiwa ili nijue kanuni na sheria iliyotumika, baada ya hapo nijue nikate rufaa kwa kosa lipi, lakini siyo kama hivi wanavyofanya TFF,” alisema Muro.

Post a Comment

 
Top