SIMBA haitaki mchezo! Wekundu hao wa Msimbazi wamejipanga kufanya kile ambacho mashabiki wao wanakihitaji na kwa kuanzia wamepanga kufanya usajili utakaotingisha nchi.
Unajua ikoje! Baada ya kuanza mazungumzo na straika wao wa zamani Mganda, Emmanuel Okwi ili kumrudisha dirisha dogo la usajili, vigogo hao wamemfungia kazi mshambuliaji wa zamani wa Azam FC, Kipre Tchetche.
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya Simba zinadai kuwa mbali na Okwi na Kipre, Wekundu hao wa Msimbazi wameanza mpambano wa kumrejesha beki wao wa zamani, Shomari Kapombe, ambaye kwa sasa anakipiga katika klabu ya Azam FC.
Kuhusu Okwi, taarifa zinadai mazungumzo yanakwenda vizuri na suala lake haliwaumizi sana kichwa Wekundu hao wa Msimbazi, kwani hana namba katika kikosi chake cha sasa cha SonderjyskE, kinachoshiriki Ligi Kuu nchini Denmark.
Taarifa zaidi kutoka ndani ya Simba zinadai kuwa kwa upande wa Kipre, ambaye anakipiga nchini Oman, wamepania kufanya kila linalowezekana ili kumng’oa na kwa jinsi Wekundu hao wa Msimbazi walivyojipanga, zoezi hilo linaweza kufanikiwa.
Kwa upande wa Kapombe, Wekundu hao wa Msimbazi wameendelea kuvutiwa na uwezo wake, ambapo wanaamini atakuwa msaada mkubwa na sasa wametega mitego kila kona kuhakikisha nyavu zao zinamnasa beki huyo, ambaye aliwahi kuichezea Simba.
Jeuri ya Simba ya kutaka kuwasajili Okwi, Kipre pamoja na Kapombe kwa wakati mmoja inatokana na kujitoa kwa hali na mali kwa mfanyabiashara maarufu na Mwanachama wao, Mohamed Dewji ‘MO.’
Dewji, ambaye kwa sasa anasubiri tu kukabidhiwa timu kutokana na kutaka kuweka hisa ya asilimia 51, amekuwa akimwaga fedha, zikiwamo zile za mishahara kwa wachezaji, akisaidiana na matajiri wengine na uongozi chini ya Rais Evance Aveva.
Kigogo mmoja ndani ya Simba aliliambia DIMBA kuwa baada ya kuteseka kwa miaka minne mfululizo, sasa wamejipanga kwa kila hali kuhakikisha wanafurahi kwa kutwaa ubingwa na kushiriki michuano ya kimataifa.

“Hayo yote yanayofanyika ni ili kurejesha furaha yetu ambayo imepotea kwa miaka minne mfululizo, uongozi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, akiwamo Mohamed Dewji, wameamua kufanya makubwa sana msimu huu,” alisema kigogo huyo.
DIMBA lilimtafuta Kipre Tchetche ili kuzungumzia suala hilo, ambapo alisema tetesi hizo zilianza kuenea hata kabla ya kwenda Oman na kwamba kwa sasa anachokiangalia ni kufanya kazi na timu ambayo anaitumikia.
“Sishangai kusikia hivyo, kwani mchezaji yeyote kuhusishwa na timu nyingine ni jambo la kawaida, taarifa hizo kama unakumbuka zilianza kuenea hata kabla ya mimi kuja huku Oman, ila niseme tu naendelea kuitumikia timu yangu mpya huku niliko,” alisema.
Kwa upande wa Okwi, alisema hawezi kuzungumzia suala lolote la kurejea Simba, kwani ana imani Simba ni klabu ambayo ilimfanya ajulikane.
“Simba ni timu ambayo imenilea na tetesi za kurudi kuichezea tena zimekuwepo kwa muda mrefu, kwa sasa sitasema chochote,” alisema Okwi.

Post a Comment

 
Top