KUFUATIA makocha wa klabu za Simba na Yanga kutoa maoni kuwa nyasi za Uwanja wa Uhuru kwamba ni hatari kwa wachezaji kutokana na ugumu wa nyasi hizo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limesema kuwa suala la timu hizo kuutumia uwanja huo katika mechi za Ligi Kuu Bara, haliwezi kukwepeka kwa kuwa ulishafanyiwa ukarabati wa kutosha ukigharimu mamilioni ya fedha.

Kocha wa Yanga, Hans van Der Pluijm na Kocha Msaidizi wa Simba, Jackson Mayanja, kila mmoja kwa wakati wake alidai kuwa sehemu ya kuchezea ya uwanja huo bado tatizo kubwa ambalo linaweza kusababisha wachezaji kupata majeraha.


Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas, alipoulizwa juu ya madai hayo alisema: “Kiukweli suala la kuutumia uwanja huo haliwezi kukwepeka kwa timu yoyote ambayo itaanza kutoa visingizio.

“Umeshakamilika na upo tayari kutumika katika michezo ya ligi kuu na lazima ifahamike wazi kwamba hao wanaosema hivyo hakuna ambaye tayari ameshaumia.

“Lakini hilo tayari lilishasemwa na Bodi ya Ligi mapema kabisa hata kabla serikali haijakabidhi, sasa haliwezi kubadilika, hivi jamani watu hawaoni Uingereza kwamba ule Uwanja wa Wembley unatumika katika mechi kubwa za heshima na ndiyo uwanja wa taifa! Tunataka utumike hivyo katika mechi kubwa pekee, tena zile za kimataifa ila zilizobakia utatumika huohuo,” alisema Lucas.

Post a Comment

 
Top