HABARI ni kuwa kuna uwezekano mkubwa wa Yanga kutomtumia beki wake, Hassan Kessy kutokana na kesi yake kuonekana kuwa kizungumkuti huku ikionekana kuwaendea vibaya wahusika hao.

Kessy alisajiliwa Yanga hivi karibuni na jina lake likapelekwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) katika orodha ya waliosajiliwa kwa msimu wa 2016/17, lakini kitendo cha Simba kugoma kutoa barua ya kumuacha, kinamaanisha kuwa hataweza kuichezea Yanga ikiwa suala hilo halitapatiwa ufumbuzi.

Katibu wa Yanga, Baraka Deusdedit, amekiri kuwa mpaka kufikia jana walikuwa hawana mamlaka ya kumtumia beki huyo kwa kuwa hawajapata barua ya Kessy kuachwa na Simba wanaotaka walipwe kwa kile walichodai alisajiliwa wakati akiwa na mkataba na Simba.

Taarifa za ndani kutoka TFF zimesema ishu hiyo ni ngumu TFF kuiingilia badala yake ni busara za Simba kuketi na mchezaji mwenyewe kulimaliza, lakini vinginevyo Yanga inaweza kuingia ‘chaka’ na akawa anaishia kufanya mazoezi tu.

“Inaonekana Yanga wanataka kuiruka kesi yenyewe, wameshaona walifanya kosa kumsajili kabla ya mkataba wake kuisha pale Simba, sasa Simba waliwataka fidia ya dola 60,000 (zaidi ya Sh milioni 120) ili watoe barua hiyo lakini Yanga hawataki.

“Wanaogopa kuzilipa maana wakithubutu tu, itazaa kesi nyingine ya kumsajili mchezaji wakati ana mkataba na timu nyingine, ndiyo maana nao wako kimya. Yote kwa yote, Kessy bila barua kutoka Simba, hawezi kuichezea Yanga popote pale,” alieleza mtoa taarifa.

Moja ya ushahidi wa Simba ni baada ya kumuona beki huyo akiwa na jezi ya Yanga, Mei 25, 2016 katika mchezo wa Kombe la FA kati ya Yanga na Azam FC huku mkataba wake na Simba ukiwa hai kwani ulikuwa unamalizika Juni 15, 2016. 

Post a Comment

 
Top