FOWADI mpya wa Simba aliye kwa mkopo, Ame Ally ‘Zungu’ amekiangalia kikosi cha timu hiyo na kutamka kuwa kwa jinsi mambo yalivyo, hana namna zaidi ya kujipanga kisawasawa kama kweli anataka kuonekana kutokana na kasi ya ajabu iliyoonyeshwa na mafowadi, Laudit Mavugo na Ibrahim Ajib kuanzia mazoezini hadi kwenye mechi.
Zungu, ametua Msimbazi akitokea Azam kwa mkopo, hata hivyo picha inayojionyesha hana nafasi kikosi cha kwanza mbele ya wakali hao ambao Jumatatu wiki hii waliwakosha mashabiki kwa kuhusika katika mabao yote manne wakati Simba ikiichapa AFC Leopards ya Kenya mabao 4-0 katika mchezo wa Tamasha la Simba Day.
Katika mchezo huo, Ajib alifunga mabao mawili huku Mavugo akifunga moja na kutengeneza jingine kwa Shiza Kichuya lakini kilichowachanganya mashabiki ni jinsi walivyoweza kuelewana vizuri katika kutengeneza mabao hayo kana kwamba wamezoeana siku nyingi.
Katika mahojiano na gazeti hili, Zungu alikiri kikosi kicho kujaa ushindani kila safu, hali inayomlazimu kujitutumua mazoezini ili kumshawishi kocha.
“Kiukweli kuna ushindani mkubwa, kila mmoja anaonekana ana ari ya ushindani na wengi wanajua, hivyo haina jinsi lazima ni kupambana kwelikweli na amini pia nafasi inaweza kupatikana japo ushindani si wa kitoto,” alisema fowadi huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar.

Post a Comment

 
Top