KIUNGO wa Azam FC, Himid Mao, jana aliingia katika matatizo baada ya kudaiwa kumkwida na kumpiga ngumi askari wa usalama barabarani maeneo ya Chanika nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Spotiripota ilipowasiliana na Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohammed Mpinga alisema amepata taarifa hizo pia.
“Ni kweli na mchezaji huyo anashikiliwa kwenye kituo cha Stakishari, lakini vizuri uzungumze na RPC wa Ilala kwa kuwa suala hilo linakwenda kwenye jinai,” alisema Kamanda Mpinga.
Akizungumzia tukio hilo ambalo inadaiwa lilitokea jana asubuhi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Salum Hamduni alikiri kutokea kwa tukio hilo ambapo alifafanua chanzo ni mwendo kasi wa gari ambayo alikuwa akiendesha mchezaji huyo.
“Ni kweli kabisa tukio hilo limetokea asubuhi ya leo (jana), huyo mchezaji wa Azam inadaiwa alikuwa katika mwendo kasi ndipo askari alipomsimamisha lakini wakati mazungumzo kati yao yakiendelea, inaonekana walipishana kauli na ndipo mchezaji huyo alipomkwida shati lake na kumtwanga ngumi ya usoni.
“Inasemekana amemjeruhi vibaya usoni na hivi sasa mchezaji huyo anashikiliwa katika Kituo cha Polisi Sitakishari kwa ajili ya mahojiano zaidi ila taarifa za kina juu ya suala hilo bado hazijanifikia ambapo kwa sasa nasubiri ripoti ya maandishi ili niweze kujua eneo sahihi lilipotokea tukio hilo, jina la mtuhumiwa ambaye ni mchezaji wa Azam pamoja na askari aliyepigwa,” alisema Hamduni.
Alipoulizwa Ofisa Habari wa Azam FC, Jaffar Idd juu ya tukio hilo alisema: “Kuna tukio limetokea kuhusu Himid, maofisa wetu wanafuatilia, watakaponipa taarifa nitakuwa na muda mzuri wa kulielezea lakini siyo kwa sasa.”

Post a Comment

 
Top