MWENYEKITI wa Yanga, Yusuf Manji, ameibuka upya baada ya juzi kutangaza kutaka kuikodi klabu hiyo kwa muda wa miaka kumi ili kuifanya kuja kuwa moja ya klabu kubwa ndani na nje ya nchi.
Juzi Jumamosi Yanga ilifanya Mkutano Mkuu wa Dharura kwa wanachama wa klabu hiyo ambapo Manji alitangaza ombi lake hilo ambalo sasa kazi imebaki kwa Baraza la Wadhamini la Klabu ya Yanga kukubali au la.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Jumapili jijini Dar, Manji alisema amepanga kufanya mambo makubwa ndani ya klabu hiyo endapo tu ombi lake hilo litakubalika, huku akiwashangaa wanachama wa klabu hiyo kwa kushindwa kumuuliza maswali katika mkutano huo.

Wanachama wasimuogope
“Unajua nilikuwa nashangaa sana kuona kila ninachokiongea hakuna hata mwanachama aliyepinga wala kuuliza swali ambalo ningeliona kweli hawa watu wanahitaji ufafanuzi.
“Wao kila nikiongea wanaitikia ndiyo, nilishangaa sana, yaani hawajauliza kwa nini nimeamua kutangaza kuikodi kwa muda wa miaka kumi na siyo mitano au 20, kutokana na hilo, ndiyo maana leo (jana) nimeamua kuwaita ninyi wanahabari kwenda kuwapa ufafanuzi wa mkutano ule.
“Siwezi kutoa ahadi moja kwa moja kwamba ndani ya miaka hiyo kumi nitafanya nini kwa Yanga kwa sababu naogopa inaweza isiwe hivyo nikaja kuonekana muongo, lakini nitaumia sana kuona sijafanikiwa halafu MO amefanikiwa na Simba yake.”

Kubadili mfumo wa uendeshaji
“Yanga kwa kipindi kirefu nilichokuwa ndani ilikuwa ikiendeshwa kwa mfumo wa hasara, tazama mwaka jana tulipata hasara ya zaidi ya bilioni 1.5 na mwaka huu tunaelekea kupata hasara ya bilioni 1.9, sasa nikija kuikodi kwa miaka hiyo kumi, hasara hizi hazitakuwa kwenye klabu bali zitakuwa zangu.
“Lakini kwa kuwa tayari nimetangaza faida itakayopatikana asilimia 75 zitakuwa zangu na 25 zinaenda kwa klabu, basi mambo yakienda kama nilivyopanga Yanga itakuja kuwa moja ya klabu kubwa hapa nyumbani na nje ya hapa.
“Tutakuwa na uwanja wetu, usafiri bora kama ndege, kuwa na benki yetu na vingine vingi ambavyo ni mahitaji muhimu kwa klabu.”

Post a Comment

 
Top