KUFUATIA lile sakata la Rais wa Simba, Evans
Aveva wiki iliyopita kukamatwa na kuhojiwa kabla ya kuachiwa kwa dhamana,
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru), imemtaka kuripoti
katika makao makuu yao kesho Jumanne ili kuendelea kuhojiwa.
Aveva alikumbwa na majanga hayo na kulala ndani
kwenye Kituo cha Polisi cha Urafiki kilichopo jijini Dar, baada ya kubainika
alifanya uchepushaji wa fedha za mauzo ya aliyekuwa straika wa timu hiyo,
Emmanuel Okwi walizolipwa baada ya kumuuza kwenye timu ya Etoile du Sahel ya
Tunisia.
Fedha hizo ambazo ni dola laki tatu, inadaiwa
zilitolewa kwenye akaunti ya Klabu ya Simba na kuhamishiwa kwenye akaunti yake
binafsi kabla ya kupelekwa kwenye akaunti nyingine iliyopo nchini Hong Kong.
Kutokana na hali hiyo, Takukuru ikahisi kuna kila
dalili za kuwepo kwa mazingira ya rushwa hivyo kuamua kulifuatilia suala hilo
ambapo lilianza kwa kumtia mikononi Aveva, kabla ya baadhi ya Wajumbe wa Kamati
ya Utendaji ya Simba nao kuitwa kwa ajili ya mahojiano.
Chanzo cha habari kilichoomba hifadhi ya jina
lake, kilisema: “Ameambiwa Jumanne ndiyo aende kujieleza tena kwenye makao
makuu ya Takukuru, hivyo kutokana na hilo kesho (leo) Jumatatu tutakuwa naye
kwenye tamasha letu la Simba Day.”
Alipopigiwa simu rais huyo, muda wote simu yake
ilikuwa haipokelewi, licha ya juhudi za mara kwa mara kumtafuta.


Post a Comment