PAMOJA na nafasi finyu waliyobakiza Yanga kufuzu hatua ya nusu fainali kwenye Kombe la Shirikisho Afrika, rekodi za kikosi hicho dhidi ya timu za Kiarabu kwenye Uwanja wa Taifa, zinaipa nafuu kubwa kuelekea mchezo wa leo Jumamosi dhidi ya MO Bejaia ya Algeria.
Takwimu zinaonyesha tangu 2009, hakuna timu kutoka Ukanda wa Afrika Kaskazini, maarufu kama nchi za Kiarabu, iliyowahi kupata ushindi pale Taifa na ushindi wao mkubwa huwa ni sare.
Mabingwa wa kihistoria Afrika, Al Ahly ya Misri, 2009 waliandikisha rekodi ya kuwa timu ya mwisho ya Kiarabu kuifunga Yanga nje-ndani ambapo waliichapa bao 1-0 pale Taifa kabla ya kuifunga tena mabao 3-0 mjini Cairo.
Ukiwa ni mwaka wa saba sasa, Yanga tayari imekutana na timu nne za Kiarabu lakini zote zimeshindwa kupata pointi tatu pale Taifa.
Mwaka 2012 ilikutana na Zamalek ya Misri ambapo zilitoa sare ya 1-1, kabla ya mwaka 2014 kuvunja rekodi kwa kuifunga timu ya Kiarabu, Al Ahly kwa bao 1-0. 2015 Waarabu wa Etoile du Saleh nao wakaangukia kwenye mkumbo wa kugawana pointi pale Taifa kwa sare ya 1-1 kabla ya kuwang’ang’ania tena Al Ahly mwaka huu kwa kufungana bao 1-1.

Post a Comment

 
Top