WAKATI Yanga ikiwa katika hatua za mwisho kucheza mechi yake ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Mo Bejaia, wachezaji wa Yanga wamelalamika kushinikizwa na baadhi ya wanachama wanaodai wanatokea katika matawi ya Yanga.
Wachezaji saba wa Yanga, wamezungumza na gazeti hili na kulalamika kuwa wamechukizwa na shinikizo kutoka kwa baadhi ya watu wanaojiita wanachama wanaotaka kuwavuruga wakiwataka kudai baadhi ya malipo yao ambayo hayajakamilika.
Mmoja wa mawinga wa Yanga, amesema kuwa kuanzia wiki iliyopita, walianza kuzungumza na watu wanaowataka kuudai uongozi kila wanachodai.
“Unajua kwa mfumo wa Yanga, hata kama ninaweza kuwa ninadai kitu, basi nawasiliana na uongozi na hiki kinamalizwa. Lakini wamekuwa wakipita na kutushauri tudai sasa kabla ya mechi ya Mo Bejaia,” alisema.
Mwingine ambaye ni beki alisema amekuwa akipata shida na imefikia watu hao waliosema wanatokea katika matawi matatu tofauti, wanamuona kuwa ni adui.
“Imefikia sasa wananiona mimi ni adui, hili si jambo sahihi. Kama ninadai basi nitafanya hivyo na inashangaza wao kutaka ninayedai nifanye hivyo wakati mimi sioni ni sawa.
“Unajua wachezaji wa Yanga kaka wamebadilika. Wanajua nini cha kufanya, kwa kifupi tumeamua kusema wajue, wasituingize kwenye mgogoro tafadhali,” alisema.
Wachezaji wengine walioungana na hao wawili, wamesisitiza wanataka kuifanya kazi yao kwa ufasaha na wasingependa kuhusishwa kwenye migogoro.
“Kama kuna tofauti zao za kiuongozi, basi wazimalizie huko. Nafikiri wanataka kututumia sisi, tufanye vibaya wapate wanachotaka, si sahihi hata kidogo.”
Championi Jumamosi lilimpata Katibu Mkuu wa Yanga, Baraka Deusdedit naye akasema uongozi wao unajua kila kitu.
“Hakuna tusichokijua, nafikiri kikubwa watu waonyeshe Yanga ni yao na kuacha kutengeneza matatizo,” alisema na kusisitiza hana muda kwa kuwa wana maandalizi ya mkutano wa dharura wa wanachama unaofanyika leo kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam.

Post a Comment

 
Top