STRAIKA wa Simba, Ibrahim Ajib, jana asubuhi kwenye mazoezi ya timu hiyo alijikuta akiliwa Sh elfu kumi bila ya kutarajia baada ya kuwekeana dau na kipa wa timu hiyo, Denis Richard.
Ishu ilikuwa hivi; Baada ya kumalizika kwa mazoezi ya asubuhi yaliyofanyika kwenye Uwanja wa Highlands mkoani hapa ambapo Simba imepiga kambi, Ajib alikuwa akisema katika penalti tano atakazompigia Denis, basi hadaki hata moja na kama akidaka japo moja basi atampa kiasi hicho cha fedha.
Championi ambalo lilikuwepo uwanjani hapo, lilishuhudia kila kitu mwanzo hadi mwisho ambapo muafaka ulifikiwa kwamba Ajib apige penalti hizo na Denis akakae langoni, jambo ambalo lilikubaliwa na kila mmoja huku wachezaji wakiwa na shauku ya kuona nini kitatokea.
Cha kushangaza na kufurahisha ni kwamba, penalti ya kwanza tu Denis akaiokoa, hivyo mchezo ukaishia hapo ambapo baada ya kuiokoa wachezaji wenzake wakamshangilia kwa nguvu huku wengine wakimbeba kutokana na kuonyesha umahiri wake wa kudaka penalti.

Post a Comment

 
Top