MTIHANI wa kwanza wa Kocha Jose Mourinho wa Manchester United kutwaa taji lake la kwanza klabuni hapo ni kesho Jumapili wakati timu yake itakapocheza mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Leicester City.
Mechi hiyo itachezwa kwenye Uwanja wa Wembley jijini London ukiwakutanisha bingwa wa Ligi Kuu England ambaye ni Leicester City na bingwa wa Kombe la FA, Man United.
Mambo mawili yanatazamwa katika mchezo huu, kwanza ni nguvu ya Leicester City katika kuendeleza ubabe wake kwa vigogo pia uwezo wa Mourinho katika soka la England akiwa na Man United.
Msimu uliopita wa Ligi Kuu England, Mourinho aliifundisha Chelsea na hakupata mafanikio kwani aliishia kufukuzwa wakati Kocha wa Leicester City, Claudio Ranieri alitwaa ubingwa.
Gumzo la mechi hii ni kuona Mourinho anavyorejea katika soka la England baada ya kuchemka msimu uliopita huku kukiwa na hatari ya kutolewa nishai na Ranieri raia wa Italia.


MAN UNITED FAIDA, HASARA LEICESTER CITY
Wakati usajili ukiendelea, inaonekana Man United ipo katika faida kwa kuwasajili nyota kama straika Zlatan Ibrahimovic, kiungo Henrikh Mkhitaryan na beki Eric Bailly huku kiungo Paul Pogba akiwa njiani kusajiliwa muda wowote.
Licha ya kwanza, Mourinho amewapa mkono wa kuondoka  nyota kadhaa wakiwemo Bastian Schweinsteiger, Adnan Januzaj na wengineo, bado Man United inaonekana ipo imara.
Yenyewe Leicester City imemuuza kiungo wake N'Golo Kante kwenda Chelsea lakini imewasajili kipa Ron-Robert Zieler kutoka Hannover 96 ya Ujerumani, beki Luis Hernández (Sporting Gijon, Hispania), kiungo Nampalys Mendy (Nice, Ufaransa) na mshambuliaji Ahmed Musa raia wa Nigeria kutoka CSKA Moscow ya Urusi.
Wachambuzi wa mambo wanaona ni kama Man United imepata faida ya kuwasajili kina Ibrahimovic kwani wamefiti moja kwa moja kikosi cha kwanza na kufanya vizuri lakini kuondoka kwa Kante kikosini Leicester City imeonekana kama tatizo.


NGUVU YA POGBA
Man United hadi sasa ipo katika hatua za mwisho kumsajili Paul Pogba kutoka Juventus ya Italia na tayari Mourinho amesema anataka kiungo huyo acheze mechi ya kesho.
Mourinho alitoa kauli hiyo mapema wiki hii akionyesha kuwa harakati za kumnasa Pogba zipo katika hatua nzuri na anaamini mchezaji huyo atakuwa msaada mkubwa kwake.

NGUVU YA LEICESTER CITY
Kama ilivyokuwa katika ligi kuu, nguvu ya Leicester City ipo katika umoja wa kucheza kwa kujituma bila ya kumtegemea mchezaji muhimu na Ranieri bado ana moyo uleule kwamba hawana la kupoteza.
“Tunaingia kucheza na timu yenye kila kitu, sisi kama ilivyo katika ligi kuu hatuna la kupoteza tutacheza kwa nidhamu ili tushinde,” anasema Ranieri.

MATAJI
Man United inacheza mechi hii ya Ngao ya Jamii ikiwa imewahi kutwaa ubingwa wake mara 20 huku mara ya mwisho kufanya hivyo ikiwa 2013, wakati Leicester City imetwaa ubingwa wake mara moja tu na mara ya mwisho ikiwa 1971.
Leicester City imecheza fainali za Ngao ya Jamii mara moja tu wakati Man United yenyewe ikiwa imecheza hatua hiyo mara 29. Katika ligi kuu, Man United imetwaa ubingwa mara 13 wakati Leicester City imefanya hivyo mara moja tu.


MAN UNITED WABABE
Katika mechi tano walizokutana Man United na Leicester City kati ya Aprili 13, 2004 na Mei Mosi, mwaka huu, Man United wameonekana kuwa wababe wakishinda mara mbili huku Leicester City wakishinda moja na kutoka sare mbili.
Katika mechi hizo, Man United imefunga mabao tisa huku Leicester City ikifunga manane hivyo kuwa na tofauti ya bao moja tu.

MAN UNITED ILIPIGWA KIPIGO KIKALI
Septemba 21, 2014 katika mchezo wa ligi kuu, Leicester City ikiwa nyumbani kwenye Uwanja wa King Power iliifunga Man United mabao 5-3 na kushangaza wengi.
Katika mchezo huo, mabao ya Leicester City yalifungwa na Leonardo Ulloa (dk 17 na 83), David Nugent (dk 62 penalti), Esteban Cambiasso (dk 64) na Jamie Vardy aliyefunga dakika ya 79. Mabao ya Man United yalifungwa na Robin van Persie dakika ya 13, Angle di María (dk 16) na Andre Herrera dakika ya 57.

MECHI TANO ZA MWISHO

Katika mechi tano za mwisho ambazo klabu hizo zimecheza hivi karibuni, Man United imeshinda nne na kufungwa moja huku Leicester City ikishinda mbili tu ikatoka sare mbili na kufungwa mara moja.
Kwenye michezo hiyo, Man United imefunga mabao 13 na kufungwa mabao manane huku Leicester City ikifunga mabao sita na kufungwa mabao saba.

Post a Comment

 
Top