KOCHA mpya wa Simba, Joseph Omog amesema yeye sera ya soka lake analolitaka ndani ya uwanja ni lile la pasi siyo mashambulizi ya ghafla yaani ‘kaunta ataki’ na anaamini atafanikiwa kwa pasi zake.
Wakati kocha huyo akitaka soka la pasi kama linalochezwa na Arsenal ya England, wapinzani wao Yanga wenyewe chini ya kocha wao Mholanzi, Hans van Der Pluijm wanacheza soka la kasi linalotegemea mashambulizi hayo ya kushitukiza.
Omog raia wa Cameroon, aliwasili nchini usiku wa kuamkia juzi akitokea kwao na jana mchana alisaini mkataba wa miaka miwili kuifundisha Simba hadi mwaka 2018.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Omog alisema sera yake kubwa ni timu yake kucheza soka la pasi nyingi za haraka wakati wakiwa na mpira wakienda kushambulia lango la timu pinzani.
Omog alisema, anaifahamu vizuri Simba ambayo aliwahi kukutana nayo mara mbili kwenye msimu wa 2013/14, hivyo ana matumaini makubwa ya kuleta mabadiliko katika msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.
Kila kocha ana sera yake katika timu, lakini kwa upande wangu mimi ninataka kuona timu yangu ikicheza soka la pasi nyingi wakati timu ikiwa na mpira tukiwa tunashambulia.
“Pia wakati timu ikiwa bila mpira, ninataka kuona wachezaji wangu wakikaba wote na hilo ndilo soka la kisasa hivi sasa, ninataka kuona tunacheza kitimu,” alisema Omog aliyewahi kuinoa Azam na kuipa ubingwa wa ligi kuu msimu wa 2014/15.
 

Post a Comment

 
Top