Ngoma
KUNA dili la straika wa Yanga, Donald Ngoma kusajiliwa na Mamelodi Sundown ya Afrika Kusini, sasa klabu yake imeelezwa kuanza harakati za kuziba nafasi yake kwa kumtaka Kipre Tchetche wa Azam FC.
Ngoma aliyetua Yanga msimu uliopita kwa kusaini mkataba wa miaka miwili na kufanya vizuri ameivutia Mamelodi ambayo imeapa kumsajili ili akaisaidie katika Ligi Kuu ya Afrika Kusini.
Mmoja wa mabosi wa Yanga mwenye nguvu kubwa ya ushawishi katika mambo ya usajili aliliambia Championi Jumamosi kuwa, kutokana na Mamelodi kuongeza nguvu ya kumuhitaji Ngoma na wao wanazungumza na Azam ili wamsajili Tchetche raia wa Ivory Coast.
Alisema lengo lao ni kupata msaada wa Tchetche katika mechi za kimataifa na msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.
“Tumewafuata Azam ili waweze kutukubalia kumsajili Tchetche ambaye bado ana mkataba wa mwaka mmoja nao, kuna masharti wametupa ili kufikia makubaliano.
“Tunataka Tchetche achukue nafasi ya Ngoma kwani kuna uwezekano mkubwa akaondoka hivyo hatutaki kupata tabu pia tunazungumza kuhusu uwezekano wa kumsajili na Pascal Wawa.
KIPRE

“Ila kuhusu Wawa bado tunavutana kwani itabidi tumuache mchezaji mwingine au iwe kwa makubaliano maalum ya mechi za kimataifa tu, naamini Azam watakubali kwa faida ya nchi.
Alipotafutwa Katibu Mkuu wa Yanga, Baraka Deusdedit alisema: “Bado mapema sana kuzungumzia suala hilo, mimi sijui inawezekana watu wa usajili ndiyo wanafahamu zaidi.”
Lakini Katibu Mkuu wa Azam, Idrissa Nassor kuhusu suala hilo, alisema: “Kwa upande wetu hatuwezi kuwazuia Yanga kuja kumsajili Tchetche kwani  soka ni mchezo wa furaha.
“Tunawakaribisha Yanga kama wanamuhitaji Tchetche tukae mezani wamsajili lakini kwa sasa hatujaona barua yao yoyote na iwapo hawatakuja basi ataendelea kuitumikia Azam.”

Post a Comment

 
Top